Loading...
ADVERTISE WITH US ON THIS BLOG.CALL +255 714 789 592/ +255 682 997 767/ +255 752 944 022

MWENYEKITI WA CCM WILAYA YA MASASI (SIMBA WA YUDA) AKANUSHA UVUMI WA KUJIUNGA NA UKAWA

TANGAZO
MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi Wilaya ya Masasi,Kazumari Malilo (Simba wa Yuda) akizungumza na wananchi wa kijiji cha Nanganga,kata ya Nanganga wilayani Masasi wakati wa uzinduzi wa kampeni za ubunge jimbo la Ndanda ambapo amekanusha yeye kujiunga na Ukawa.

Na Mwandishi Wetu:Masasi.
MWENYEKITI wa chama cha mapinduzi wilaya ya Masasi Kazumari Malilo (Simba wa Yuda) amekanusha vikali uongo na uzushi uliokuwa umezagaa kwa siku za hivi karibuni wilayani humo kuwa yuko mbioni kujiunga na umoja wa vyama vinavyounda ukawa kwa madai ya kumfuata rafiki yake aliyehamia huko baada ya kubwagwa kwenye mchakato wa kura za maoni ndani ya chama.

Aliyasema hayo jana wakati wa uzinduzi wa kampeni za chama hicho kwenye jimbo la Ndanda mkutano uliofanyika kwenye kijiji cha Nanganga wilaya ya Masasi ambapo alisema taarifa hizo zilizosambazwa na wale aliowaita ni  wapinzani wake wa muda mrefu kwenye medani za kisiasa kuwa ni za uongo na uzushi zenye lengo la kudhoofisha harakati zake za kukirudisha chama cha mapinduzi madarakani.

Alisema ni kwa muda mrefu sasa amekuwa akisikia uzushi huo mitaani wa yeye kutaka kuhama CCM na kuhamia Ukawa baada ya mgombea wa jimbo hilo aliyekuwa anaomba ridhaa kutoka kwa wana CCM aweze kupeperusha bendera ya chama hicho Cesil Mwambe kubwagwa kwenye mchakato wa kura za maoni ndani ya chama na Mariam Kasembe.

Alisema ni kweli Cesil Mwambe alikuwa mtu wake wa karibu lakini ukaribu huo ulitokana na yeye kuwa mwanachama wa chama cha mapinduzi lakini urafiki huo umekufa na kuzikwa rasmi baada ya yeye kuhamia Chadema  huku akifananisha kitendo kilichofanywa na mgombea huyo kuwa ni sawa na “Kuuza panya msikitini” ambapo  alimtaka kusahau ndoto zake za kuwa mbunge wa jimbo la Ndanda na kwamba atahakikisha haibuki kidedea kwenye uchaguzi huo.

“Watu wamekuwa wakinizushia uongo kuwa mimi Malilo nataka kuhama CCM na kuhamia Chadema kumfuata Cesil Mwambe…natangaza rasmi mbele yenu kuwa sikuwahi kufikiria kuwa na mpango huo na sina mpango huo yeye kama amehama ni uroho wake wa madaraka na naomba kwa mungu wote waliotumika katika kusambaza uongo huo walaaniwe duniani na mbinguni”.alisema Malilo huku akiomba dua kwa dini yake ya kiislam.

Alisema wako baadhi ya wanachama wa chama cha mapinduzi walioenda kwa mgombea wa nafasi ya ubunge jimbo la Ndanda kwenda kutoa taarifa kuwa yeye mwenyekiti wa CCM wilaya ya Masasi hawezi kumuunga mkono Mariam Kasembe kitendo ambacho amekilaani hadharani na kwamba yupo tayari kumpigia debe mgombea huyo wa CCM huku akijinasibu kuwa chama chake kitaibuka kidedea.

Aidha Malilo alionesha wazi kuchukizwa na vitendo alivyoviita kuwa ni vya kihuni na kejeli kutoka kwa mwanachama wa chama hicho Constancia Ng’ombo aliyebwagwa kwenye kura za maoni kwa nafasi ya udiwani kata ya Ndanda ambaye amekuwa akisambaza uvumi kuwa uongozi wa CCM wilaya ulichangia yeye kuangushwa kwenye nafasi hiyo mazingira yaliyopelekea kuhamia Chadema.

Alisema wanachama wote wilayani humo waliohamia chadema akiwemo mwenyekiti wa umoja wa vijana kata ya Nanganga Sadati Muhidini pamoja na wagombea wawili walioangushwa kwenye mchakato wa kura za maoni ndani ya chama akiwemo Cesil Mwambe na Constancia Ng’ombo wamefilisika kisiasa na kilichowapeleka huko ni uroho wa madaraka.

Alisema chama cha mapinduzi wilaya ya Masasi kitashinda kwa kishindo kwa nafasi zote za ubunge na udiwani na kwa kudhihirisha hilo tayari CCM imeshapita bila kupingwa kwenye kata mbili za Chikoropola na Lupaso na kwamba kwa kata zote zilizobaki uwezo wa kushinda ni mkubwa ambapo aliwaomba wanachama wa chama hicho kushikamana hasa katika kipindi hiki cha uchaguzi.


TANGAZO
Facebook Blogger Plugin by WAYEGE CO.LTD
Newer Posts Older Posts
© Copyright Mtazamo Mpya | Designed By FAHARI YA TANZANIA
Back To Top