Loading...
ADVERTISE WITH US ON THIS BLOG.CALL +255 714 789 592/ +255 682 997 767/ +255 752 944 022

CHUACHUA ATANGAZA NEEMA KWA WAKULIMA,WAFANYABIASHARA NDOGONDOGO NA WAFANYAKAZI

TANGAZO
 MGOMBEA wa nafasi ya ubunge jimbo la Masasi Rashid Chuachua akiwahutubia wananchi na wanachama wa chama cha mapinduzi waliojitokeza kwenye mkutano wa uzinduzi wa kampeni za ubunge pamoja na udiwani katika jimbo la Ndanda zilizofanyika leo kwenye viwanja vya shule ya msingi Sululu.

Na Clarence Chilumba,Masasi.
MGOMBEA wa nafasi ya ubunge kupitia chama cha mapinduzi jimbo la Masasi Rashid Chuachua amewaomba wanachama na wananchi wa jimbo hilo kumchagua ili aweze kuboresha sekta ya kilimo kwa kurasimisha ardhi ya wakulima waweze kupata hati za kimila zitakazowawezesha kupata mikopo kwenye taasisi za kifedha nchini.

Pia ametoa matumaini mapya kwa wafanyakazi wa sekta ya umma hususani walimu kwa kuwaahidi kuwa endapo watamchagua na kuwa mbunge wa jimbo hilo atahakikisha wanalipwa stahili zao ikiwemo malimbikizo ya mishahara kwa wale walimu waliopanda madaraja sambamba na kutoa mafunzo kazini kwa walimu hao.

Aidha katika mkutano huo uliohudhuriwa na viongozi pamoja na wanachama wa chama cha mapinduzi wakiongozwa na katibu wa chama hicho mkoa wa Mtwara Shaibu Akwilombe,mgombea huyo aliweka wazi vipaombele vyake kuwa ni pamoja na uchumi na uzalishaji,huduma za jamii pamoja na namna atakavyoshughulikia kero mbalimbali zinazowakabili wananchi wa jimbo la Masasi.

KATIBU wa chama cha mapinduzi mkoa wa Mtwara Shaibu Akwilombe (kulia) akimnadi mgombea wa chama hicho kwa nafasi ya ubunge jimbo la Masasi Rashid Chuachua kwa wananchi.

Akihutubia leo maelfu ya wanachama  wa CCM na wananchi wakati wa uzinduzi wa kampeni za chama cha mapinduzi kwa nafasi ya ubunge na udiwani kwa jimbo la Masasi zilizofanyika katika kijiji cha Sululu halmashauri ya mji wa Masasi alisema anafahamu kero walizonazo wananchi wa jimbo la Masasi ikiwemo maji,elimu na afya na kwamba wakimchagua kero hizo zitabaki kuwa historia.

Alisema sekta ya elimu ambayo yeye ameifanyia kazi kwa takribani miaka 15 akiwa mwalimu ina changamoto nyingi jimboni humo kama vile kuwepo kwa idadi ndogo ya wanafunzi wanaojiunga kidato cha tano pindi wanapomaliza kidato cha nne huku akitolea mfano kuwa kila mwaka wanafunzi 1800 humaliza elimu ya sekondari na wengi wao hushindwa kuendelea ma masomo ya kidato cha tano.

Alisema ili kukabiliana na tatizo hilo la wanafunzi wengi kutojiunga na kidato cha tano atahakikisha kwa kushirikiana na wizara yenye dhamana ya elimu baadhi ya shule za sekondari za kata zikarabatiwe na kuongeza majengo na miundo mbinu ya kisasa ikiwemo maji na umeme ili ziweze kuwa za kidato cha tano na sita ili kupunguza wimbi la wanafuzni wanaomaliza sekondari na wakishindwa kuendelea na masomo ya kidato cha tano.

Aidha amehaidi kushughulikia matatizo ya watumishi wa sekta ya afya ambao wamekuwa wakishindwa kupewa stahili zao kwa wakati licha ya umuhimu wa kazi yao kwa jamii huku akiweka wazi dhamira yake ya kuwa mbunge mwenye nia thabiti ya kupambana na umaskini wa kipato unaowakabili wananchi wa jimbo la Masasi.

Akizungumzia mikakati yake ya kuinua sekta ya kilimo Chuachua alisema atahakikisha pembejeo za kilimo zinawafikia wakulima kwa wakati,kusimamia bei ya mazao kwa wakulima pamoja na kutafuta masoko yenye tija sambamba na kujenga maghala makubwa na ya kisasa ya kuhifadhia chakula kama akiba ili wakati wa upungufu wa chakula jimboni humo wananchi waweze kununua kwa bei nafuu.

Alisema kwa kushirikiana na mtandao wa wakulima vijijini MVIWATA atahakikisha wakulima waliojiunga pamoja kwenye vikundi vya uzalishaji mali wanapatiwa mafunzo yenye tija kwao yatakayosaidia kuinua kipato chao mazingira yakayosaidia kuondokana na umaskini ambao amejinadi endapo atapewa ridhaa na wana Masasi basi suala hilo kwao litamalizika.
 BAADHI ya viongozi waandamizi wa chama cha mapinduzi wilaya ya Masasi wakiwa kwenye uzinduzi wa mkutano wa kampeni za nafasi ya ubunge na udiwani wa chama hicho uzinduzi uliofanyika hii leo kwenye viwanja vya shule ya msingi Sululu,Halmashauri ya mji wa Masasi.
 Wanachama wa chama cha mapinduzi wakiwa wamebeba mabango yenye ujumbe wakiwa kwenye viwanja vya shule ya msingi Sululu wakati wa uzinduzi wa kampeni za ubunge na udiwani wa chama hicho.


“Nafahamu kuwa wakulima wengi wa jimbo la Masasi hawana uwezo wa kukopa fedha kwenye taasisi zinazotoa mikopo kwa sababu hawakopesheki kwa kuwa wamekosa sifa…nitahakikisha mashamba yote ya wakulima yanarasimishwa ili mpate hati miliki za kimila zitakazowawezesha kukopa fedha benki  ili mboreshe maisha yenu na ya familia zenu”.alisema Chuachua aliyeshangiliwa na wananchi hao wakati wote.

Aidha ameonya endapo wananchi  wa jimbo la Masasi watamchagua na kuwa mbunge wao basi atakula sahani moja na maofisa wa ushirika ambao kwa namna moja ama nyingine wanasababisha kero za wakulima jimboni humo huku akisisitiza umuhimu wa kufanya ukaguzi wa hesabu za mara kwa mara kwa vyama vya ushirika kwani hivyo ndivyo vinavyochangia kuzorotesha maendeleo ya wakulima.

 BAADHI ya wanachama wa CCM wakifuatilia kwa makini vipaombele vya mgombea wa nafasi ya ubunge jimbo la Masasi Rashid Chuachua wakati wa uzinduzi wa mkutano wa kampeni.
 Rashid Chuachua akimwaga sera kwa wananchi wa jimbo la Masasi waliojitokeza kumsikiliza hii leo katika kijiji cha Sululu.

Kuhusu sekta ya uchumi Chuachua alisema mji wa Masasi ni kitovu cha biashara kwa sasa huku baadhi ya wakazi wa mji huo wakifanya  biashara  ndogondogo zisizo na tija kwao wakiwemo madereva bodaboda pamoja na mama lishe na kwamba nia yake ni kuboresha biashara hizo kwa kuwapa mafunzo ya ujasiliamali ili waweze kuunda vikundi vitakavyowawezesha kupata mikopo ya kuboresha biashara zao.

Jimbo la Masasi lina kata 14 likiwa ndani ya halmashauri ya mji wa Masasi huku jumla ya   wagombea wanne kutoka kwenye vyama vya CUF, NLD, CHADEMA pamoja na CCM wamejitokeza kwenye mtifuano huo wa kutafuta mgombea mmoja atakayekuwa mwakilishi wa wananchi wa jimbo hilo.


 Bibi akifurahia jambo wakati wa uzinduzi wa kampeni za CCM kwa nafasi za ubunge na udiwani kwa jimbo la Masasi kwenye viwanja vya shule ya msingi Sululu halmashauri ya mji wa Masasi.
 WANACHAMA wa chama cha mapinduzi wakiwa kwenye viwanja vya uzinduzi wa kampeni
Wanachama wa CCM wakiwa kwenye viwanja vya shule ya msingi Sululu wakisikiliza sera kutoka kwa mgombea wa nafasi ya ubunge jimbo la Masasi Rashid Chuachua.
TANGAZO
Facebook Blogger Plugin by WAYEGE CO.LTD
Newer Posts Older Posts
© Copyright Mtazamo Mpya | Designed By FAHARI YA TANZANIA
Back To Top