Loading...
ADVERTISE WITH US ON THIS BLOG.CALL +255 714 789 592/ +255 682 997 767/ +255 752 944 022

MGOMBEA AHAIDI KUJENGA VIWANDA VYA KUBANGUA KOROSHO MIKOA YA LINDI NA MTWARA,ATAJA VIPAOMBELE VYAKE

TANGAZO
Mgombea wa nafasi ya urais kupitia ACT-Wazalendo Mama Anna Mghwira akiwa kwenye  moja ya mikutano yake.

Na Clarence Chilumba,Masasi.
Mgombea wa nafasi ya Urais kupitia chama cha ACT-Wazalendo Anna Mghwira amesema endapo atachaguliwa na kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania atahakikisha anajenga viwanda vya ubanguaji wa korosho katika mikoa ya Lindi na Mtwara.

Aliyasema hayo jana wakati akiomba kura kwa wananchi wa mji wa Masasi kwenye mkutano wake wa kampeni uliofanyika kwenye viwanja vya Terminal two mjini humo ambapo alisema ili kurudisha thamani ya zao la korosho serikali yake itajenga viwanda vya kubangua zao hilo na kufufua vile ambavyo kwa sasa havifanyi kazi.

Alisema ili nchi iwe na maendeleo serikali yake itahakikisha kuna kuwa na uchumi shirikishi ambao hutoa fursa kwa wananchi wote kushiriki kwenye maamuzi magumu ya serikali ikiwemo ujenzi wa viwanda,ubinafsishaji wa rasilimali za taifa na kwamba ni lazima serikali yake itawashirikisha wananchi wenyewe waweze kukubali ama vinginevyo.

Alisema maeneo mengi aliyopita kwenye mikoa ya kusini wakati wa kampeni zake amejionea ardhi nzuri yenye rutuba inayofaa kwa kilimo na kwamba endapo watanzania watampa ridhaa ya kuongoza nchi serikali yake itaboresha kilimo kwa mikoa ya kusini kwa kuleta pembejeo na zana za kilimo kwa wakati na kwa gharama ndogo.

Kwa mujibu wa mgombea huyo wa nafasi ya urais alisema sekta ya kilimo imekuwa haipewi kipaombele mazingira yanayosababisha wakulima bado kuendelea kutumia zana duni za kilimo ambapo amehaidi kushughulikia kero hizo endapo watanzania watampa ridhaa ya kuongoza.

Aidha Mghwira alisema ataboresha mifuko ya hifadhi ya jamii ili kila mwananchi awe na akiba tofauti na ilivyo sasa kwamba ni watumishi wa umma pekee ndio wenye akiba kupitia mifuko hiyo sambamba na kutoa huduma bora kwa wazee ili nao wanufaike na matunda ya uhuru wa nchi yao.

Mghwira alivitaja vipaombele vyake kuwa ni pamoja na hifadhi ya jamii,uchumi shirikishi,afya,elimu,miundombinu na maji huku akijinasibu kuwa serikali yake itakuwa ya uadilifu,utu na uzalendo kwa wananchi wote na kwamba wafanyakazi wa umma wanapaswa kutenda haki kwa wananchi wanaowahudumia.

Kwa upande wake mgombea mwenza wa nafasi ya urais kupitia chama cha ACT-Wazalendo Ahmad Yusuph alisema watasimamia rasilimali za nchi zilizopo ili ziweze kuleta manufaa kwa taifa na kwa wananchi kwa ujumla na kwamba moja ya  mipango yao ni kuboresha bei za mazao ya wakulima nchini.

Alisema nchi ya Tanzania ina rasilimali za kutosha kinachokosekana ni usimamizi wa rasilimali hizo ili kila Mtanzanzia aweze kunufaika na mgawanyo wa rasilimali hizo na kwamba serikali yao chini ya chama cha ACT-Wazalendo kitafanya mapinduzi katika sekta hiyo kwa kutoa fursa sawa kwa watanzania wote.


TANGAZO
Facebook Blogger Plugin by WAYEGE CO.LTD
Newer Posts Older Posts
© Copyright Mtazamo Mpya | Designed By FAHARI YA TANZANIA
Back To Top