Loading...
ADVERTISE WITH US ON THIS BLOG.CALL +255 714 789 592/ +255 682 997 767/ +255 752 944 022

MFUKO WA PENSHENI KWA WATUMISHI WA UMMA (PSPF) SASA KUKOPESHA NYUMBA NA VIWANJA KWA WANACHAMA WAKE

TANGAZO
Meneja wa PSPF mkoa wa Mtwara Omari Kaliko akizungumza na watumishi wa vyuo vya maendeleo ya wananchi mkoa wa Mtwara ambavyo ni Mtawanya,Newala na Masasi wakati wa mkutano wa baraza la wafanyakazi wa vyuo hivyo uliofanyika jana kwenye ukumbi wa chuo cha maendeleo ya wananchi Masasi.

Na Clarence Chilumba; Masasi.
Mfuko wa pensheni kwa watumishi wa umma PSPF umedhamiria kutoa huduma bora  kwa wanachama wake kwa lengo la kuboresha maisha yao pindi wanapokuwa kazini na hata mara baada ya kustaafu ikiwa ni utekelezaji wa sera na mikakati ya serikali katika kuboresha maisha ya wafanyakazi wake.

Akizungumza jana wakati anawasilisha mada ya majukumu ya mfuko wa PSPF kwenye mkutano wa  baraza la wafanyakazi wa vyuo vya maendeleo ya wananchi mkoa wa Mtwara,meneja wa PSPF mkoa wa Mtwara Omari Kaliko alisema kwa sasa mfuko huo unatoa mikopo ya nyumba na viwanja kwa wanachama wake.

Alisema PSPF inatambua umuhimu wa wanachama wake kumiliki nyumba ambapo mwanachama atakuwa analipa kidogo kidogo kwa muda wa miaka 25 mkopo utakaomwezesha mwanachama kuishi kwenye nyumba yake mara tu makato ya mkopo huo  yatakapoanza.

Alisema kwa sasa PSPF tayari imeshajenga nyumba kwa ajili ya kukopesha  wanachama wake katika maeneo ya Chanika jijini Dar es salaam nyumba ambazo hukopeshwa kwa shilingi 60 hadi 84 milioni na kwamba kwa  upande wa mikoani nyumba moja hukopeshwa kwa shilingi milioni 60 hadi 70.

Aidha Kaliko alisema licha ya mikopo ya nyumba pia PSPF inatoa mikopo mbalimbali kwa wanachama wake ikiwemo mikopo ya viwanja,elimu,mikopo kwa waajiriwa wapya pamoja na mikopo kwa wastaafu yenye masharti nafuu  ambapo kwa mkoa wa Mtwara PSPF tayari wana viwanja vilivyopimwa katika eneo la Mitengo na mji Mwema mkoani humo.

Kwa mujibu wa meneja huyo wa mkoa wa Mtwara alisema PSPF inathamini michango ya wanachama wake kwa kuwekeza katika maeneo mbalimbali huku akijinasibu kuwa mfuko huo ni tofauti kabisa na mifuko mingine ya hifadhi ya jamii kwa kuwa mwaka 2013 mfuko ulipata tuzo ya kuwa mfuko wa kwanza nchini kutoa huduma ya mikopo ya nyumba za makazi kwa wanachama wake.

Alisema ili kulipa mafao bora PSPF imekuwa ikihakikisha michango ya wanachama wake inalindwa dhidi ya mfumuko wa bei na kushuka kwa thamani ya shilingi kwa kuwekeza kwenye vitega uchumi vya muda mrefu ikiwemo majengo,hisa na dhamana za serikali na kwamba kwa sasa baadhi ya vitega uchumi hivyo ni pamoja na jengo lenye ghorofa 35 ambalo ni refu kuliko yote Afrika mashariki na kati lililozinduliwa hivi karibuni na Rais Kikwete.

“Ndugu zangu wanachama na msio wanachama  mfuko wetu wa PSPF umekuwa ukiimarika siku hadi siku…kiasi kwamba tumeweza kuwekeza katika maeneo mengi nje na ndani ya nchi ninachowaomba ni kuendelea kutuunga mkono na muachane na uvumi wa kuwa PSPF inaelekea kufilisika”.alisema Kaliko.

Akizungumzia kuhusu mpango mpya wa kuchangia kwa hiyari alisema mpango huo umeanzishwa ili kukidhi haja kwa watanzania wote ambao ni waajiriwa na wasioajiriwa na kwamba anayehitaji kujiunga na utaratibu huo anaweza kuchangia kiasi chochote alichonacho kinachoanzia shilingi 10,000 ambapo anaweza kuchangia kwa siku,mwezi na hata mwaka kadri anapopata pesa.

Mkutano wa baraza la wafanyakazi wa vyuo vya maendeleo ya wananchi  mkoani Mtwara umefanyika jana mjini Masasi kwenye ukumbi wa chuo cha maendeleo ya wananchi Masasi  na kuhudhuriwa na wajumbe kutoka katika vyuo vya Mtawanya,Newala na Masasi wakiwa wenyeji huku mada mbalimbali kutoka kwa watalamu mbalimbali zikiwasilishwa.



TANGAZO
Facebook Blogger Plugin by WAYEGE CO.LTD
Newer Posts Older Posts
© Copyright Mtazamo Mpya | Designed By FAHARI YA TANZANIA
Back To Top