Loading...
ADVERTISE WITH US ON THIS BLOG.CALL +255 714 789 592/ +255 682 997 767/ +255 752 944 022

TATIZO LA WATOTO WA KIKE MIKOA YA LINDI NA MTWARA KUKATISHA MASOMO KUTOKANA NA MIMBA LAPUNGUA

TANGAZO
Waziri wa elimu na mafunzo ya ufundi (Mbunge) Dkt.shukuru Kawambwa (picha ya maktaba).



 Lengo la mradi ni kufikia wasichana 10,200 kwa mikoa ya Lindi na Mtwara
Tatizo la watoto wa kike mkoani Mtwara kukatisha masomo kutokana na sababu mbalimbali limepungua kwa kiasi kikubwa, baada ya uwapo wa mradi wa `Hakuna wasichoweza’ unaoendeshwa na T-Marc kwa ufadhili wa Vodacom Foundation.

 Mradi huo umeonyesha mwelekeo wa kutatua matatizo yanayowakabili watoto wa kike kutotimiza wajibu wao wa masomo shuleni ikiwa ni pamoja na kutotimiza ndoto zao sambamba na kupunguza utoro. 

Akizungumza wakati wa mrejesho wa mwenendo wa mradi huo kwa wadau wa elimu wa Mkoa wa Mtwara, Meneja wa mradi huo, Doris Chalambo, alisema mradi huo ulioanza kutekelezwa mwaka 2013 mkoani humu, ulilenga kufikia wanafunzi 10,200 wa shule za msingi kuwapatia elimu ya afya, namna ya kujisitiri wakati wa siku zao na kupatiwa vifaa vya kujisitiri.

Alisema katika thamini yake iliyotolewa chini ya utekelezaji wake kwa mkoani Mtwara, umeonyesha kuwa na mafanikio makubwa baada ya kupunguza tatizo la utoro.

“Lengo la mradi ni kufikia wasichana 10,200 kwa Mikoa ya Lindi na Mtwara, lakini kwa Mkoa wa Mtwara wanafunzi wapatao 7,077 tayari wamefikiwa na tumekuwa tukiwapatia elimu juu ya wanapokuwa kwenye siku zao itakayomsaidia anapokuwa katika hali hiyo afanye kitu gani pamoja na elimu ya afya na madhara ya mimba za utotoni sambamba na kumsaidia vifaa vya kujisitiri na hii ni kutokana na kuwa suala hilo halizungumziwi kabisa katika jamii yetu hivyo mtoto anapata changamoto na kumsababishia kukosa shule kati ya siku mbili hadi tano ndani ya mwezi mmoja na kumrudisha nyuma kielimu,” alisema Chalambo.

Aidha, alisema changamoto wanazokumbana nazo katika kutekeleza mradi huo ni pamoja na baadhi ya shule kukosa miundombinu kama vyoo na chumba maalum kwa ajili ya kusaidia wasichana katika masuala ya afya  na kuwa mradi huo unatekelezwa kwa awamu mbili ikiwa awamu ya pili itakuwa mkoani Lindi.

“Katika kutekeleza mradi huu, hatuwezi kufanikiwa bila ya miundombinu, tumegundua shule nyingi vyoo siyo vizuri kwa hiyo bila kuendana na miundombinu sahihi hatuwezi kufanikiwa,” alisema Chalambo.

Akizungumza kwa niaba ya katibu tawala Mkoa wa Mtwara, Jose Kitenana, alisema mradi huo umeleta mabadiliko katika mkoa huo na kuwa serikali imekuwa ikifanya kila jitihada kuhakikisha miundombinu ya shule inakuwa rafiki.

“Mpango huu ni mzuri na kwa sisi serikali hatuwezi kufanya kila jambo, hivyo kuna wadau tunashirikiana nao kama T-Marc kutoa elimu ya afya kwa wanafunzi kwa udhamini wa Vodacom Foundation ili kusaidia watoto wetu wa kike na suala la miundombinu bado zipo taratibu zinazofanyika kuhakikisha wanajengewa mazingira rafiki,” alisema Kitenana.

Naye Mkuu wa Vodacom Foudation, Renatus Rwehikiza, alisema wamekuwa wakitoa misaada mbalimbali kwenye jamii katika vipengele tofauti na sasa wanatekeleza mradi wa `hakuna wasichoweza’ kwa lengo la kuongeza mahudhurio ya watoto shuleni na kuwa itapunguza kasi ya magonjwa, utoro na mimba za utotoni.

Mmoja wa wanafunzi, Doreen Mvungi, alisema mradi huo umewapa maarifa namna ya kukabiliana na changamoto walizokuwa wakizipata pindi wanapokuwa kwenye siku zao.

CHANZO: NIPASHE.


TANGAZO
Facebook Blogger Plugin by WAYEGE CO.LTD
Newer Posts Older Posts
© Copyright Mtazamo Mpya | Designed By FAHARI YA TANZANIA
Back To Top