Loading...
ADVERTISE WITH US ON THIS BLOG.CALL +255 714 789 592/ +255 682 997 767/ +255 752 944 022

MKUU WA WILAYA AHIMIZA WATENDAJI WA SERIKALI KUWA NI NIDHAMU KAZINI,WAFANYE KAZI KWA BIDII

TANGAZO



Na Clarence Chilumba,Masasi.
Mkuu wa wilaya ya Masasi mkoani Mtwara Bernald Nduta amewataka watendaji wa serikali kuwa na nidhamu kazini ikiwa ni pamoja na kuwahi kazini,kutenda haki kwa wananchi wanaowahudumia ili kuondoa malalamiko ya wananchi kwa serikali yao.

Wito huo ameutoa wakati anafungua mkutano wa baraza la wafanyakazi wa vyuo vya maendeleo ya wananchi mkoani Mtwara kwenye ukumbi wa chuo cha maendeleo ya wananchi Masasi ambapo alisema baadhi ya watendaji wa serikali waliopewa dhamana wamekuwa wakifanya kazi kwa mazoea.

Alisema ili Taifa la Tanzania lisonge mbele kimaendeleo ni lazima watendaji wa serikali wafanye kazi kwa bidii kwani wao ndio dira na muongozo katika maeneo yao ya kazi lakini hali ni tofauti na ilivyo sasa kwani watendaji wengi wamekuwa ndio kikwazo cha maendeleo kwa kutumia muda mwingi kufanya mambo yao binafsi.

Alisema watendaji wengi wa serikali na wananchi kwa ujumla kila uchao wamekuwa wakiilalamikia serikali huku wao wakishindwa kutimiza wajibu wao kwa taifa ambapo alisema baadhi ya nchi ambazo hii leo watanzania wengi wamekuwa wakidai zina maendeleo kuliko Tanzania ukweli ni kwamba wananchi wake wamekuwa wakifanya kazi kwa bidii.

“Ndugu zangu watumishi wa umma mliopewa dhamana ya kuwatumikia wananchi na taifa letu…kwa mfumo huu wa maisha tulionao watanzania wengi kamwe hatuwezi kupiga hatua kimaendeleo na kila siku tutabaki kuilalamikia serikali kuwa haifanyi kazi wakati sisi wenyewe ni sehemu ya serikali”alisema Nduta.

Awali akimkaribisha mkuu wa wilaya kuzungumza na wafanyakazi hao,mkuu wa chuo cha maendeleo ya wananchi Masasi Fred Mwakagenda alisema baraza hilo la wafanyakazi ni la aina yake kufanyika kwa kuwa mara nyingi hufanyika kikanda ambapo ni wawakilishi wachache huweza kuhudhuria tofauti na hivo lilivyofanyika kwa kuwa limetoa fursa kwa wafanyakazi wote kushiriki.

Alisema lengo la baraza hilo ni kujifunza masuala mbalimbali kutoka kwa wataalamu watoa mada,kujenga mahusiano miongoni mwa wafanyakazi,kubadilishana uzoefu uliopo pamoja na kuangalia kwa pamoja fursa zilizopo na changamoto zilizopo ili wafanyakazi waweze kufanya kazi kwa moyo wa kizalendo.

Kwa mujibu wa Mwakagenda alizitaja changamoto kadhaa zinazovikabili vyuo vya maendeleo ya wananchi mkoani Mtwara kuwa ni pamoja na ukosefu wa fedha za uendeshaji (Ruzuku) kutoka wizarani,ucheleweshaji wa kulipwa madai mbalimbali kwa watumishi wa vyuo hivyo,ucheleweshaji wa kupanda madaraja pamoja na watumishi wapya kutopata mafunzo maalumu pindi wanapoanza kazi.

Alisema ni vyema serikali ikaangalia kwa undani zaidi malalamiko yao ambayo mengi ni ya muda mrefu ili kurejesha imani kwa watumishi hao wa vyuo vya maendeleo ya wananchi ambavyo hufundisha stadi mbalimbali kwa vijana wengi ili waweze kujiajiri kwenye sekta binafsi na kuachana na dhana ya kuitegemea serikali katika kutoa ajira.

Mkutano huo wa baraza la wafanyakazi wa vyuo vya maendeleo ya wananchi  mkoa wa Mtwara ulihudhuriwa na wafanyakazi kutoka vyuo vya Mtawanya,Newala na Masasi huku mada mbalimbali zikiwasilishwa kutoka kwa wataalamu wa mifuko ya hifadhi ya jamii ikiwemo PSPF,NSSF na NHIF,wataalamu wa tume ya usuluhishi na uamuzi wa migogoro kazini (CMA) pamoja na maofisa wa TUGHE mkoa wa Mtwara.


TANGAZO
Facebook Blogger Plugin by WAYEGE CO.LTD
Newer Posts Older Posts
© Copyright Mtazamo Mpya | Designed By FAHARI YA TANZANIA
Back To Top