Loading...
ADVERTISE WITH US ON THIS BLOG.CALL +255 714 789 592/ +255 682 997 767/ +255 752 944 022

MWALIMU RUANGWA AKUTA JENEZA NJE YA NYUMBA YAKE,WANAKIJIJI WADAI AONDOKE HARAKA..

TANGAZO
 Na Clarence Chilumba,Ruangwa.
Katika hali isiyokuwa ya kawaida na ya kustaajabisha mwalimu mkuu  wa shule ya Msingi Mkutingome,kata ya Mbekenyera Halmashauri ya wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi Hemed Ismail Nambea amekuta jeneza likiwa limefunikwa shuka nyeupe katikati ya mlango  nje ya nyumba yake.
Jeneza lililotumika na kuwekwa nje ya nyumba ya mwalimu huyo  ni  hilo hilo ambalo hutumika kwa ajili ya shughuli za  mazishi ya kawaida kijijini hapo ambapo watu hao wanadaiwa kwenda kulichukua jeneza hilo msikitini usiku.
Tukio hili limetokea usiku wa kuamkia leo kijijini hapo kwa kile kinachodaiwa kuwa mwalimu huyo  kushindwa kwake  kuzuia suala la wanafunzi wa shule hiyo kudondoka ovyo wakiwa shuleni huku wazazi wa watoto hao wakidai kuwa chanzo cha tatizo hilo ni yeye wakiwa na imani za kishirikina dhidi ya mwalimu huyo.
Tuhuma zingine ambazo wananchi wa kijiji cha Mkutingome wanamtupia mwalimu huyo ni kwamba tatizo la watoto wao kuendelea kusumbuliwa na ugonjwa huo kunachangiwa nay eye ingawa walishindwa kueleza ni kwa namna gani mwalimu huyo anakwamisha zoezi la wanafunzi hao kupewa dawa za tiba za asili na hatimaye kupona.
Ugonjwa huo wa ajabu  kwa mara ya kwanza uliibuka shuleni hapo mwanzoni mwa mwaka jana ambapo licha ya juhudi kubwa zilizofanywa na walimu hao kutoa elimu kwa wanakijiji hao lakini bado baadhi ya wazazi wa watoto hao wamekuwa wakiwatupia lawama walimu hao.
Akizungumza na Blog ya Mtazamo Mpya hii leo Mwalimu huyo alisema kuwa ni kwa muda mrefu sasa amekuwa akiishi kwa shida na hofu kijijini hapo kutokana na vitisho vya kuuawa anavyopewa na wana kijiji hao mazingira yanayopelekea kushuka kwa morari yake ya utendaji kazi zake za ufundishaji.
Alisema kutokana na tatizo hilo uongozi wa shule hiyo pamoja na uongozi wa serikali ya kijiji walifanya kikao shuleni hapo wiki iliyopita ili kujadili mustakabali wa wanafunzi  sita ambao bado tatizo la kuanguka linawakabili na makubaliano yakawa ni kuwaondoa kwa muda wanafunzi hao shuleni hapo ili wakapate tiba.
Kwa mujibu wa mwalimu huyo alisema wiki moja iliyopita April 16 mwaka huu majira ya saa 3:00 usiku  akiwa anajiandaa kwenda kuangalia mechi kati ya timu ya Barcelona na PSG  alikuta maneno ya makali mlangoni pake  ya kumtahadharisha yaliyosema “Hatuna imani na wewe mwalimu mkuu juu ya uangukaji wa watoto shuleni kwa hiyo tunakupa siku mbili uamishe kambi bila ubishi na ukiwa mbishi utakachokiona usishangae tumechoka na mambo yako”.
Alisema baada ya kuona maneno hayo yaliyomtisha alitoa taarifa kwa uongozi wa serikali ya kijiji ambapo alihaidiwa na ofisa mtendaji wa kijiji hicho kuwa tatizo lake watalishughulikia kwa kuwatafuta wote waliohusika na kufanya kitendo hicho ambacho si cha kiungwana.
Aidha mwalimu huyo alidai kuwa huku akisubiri hatima ya suala hilo la kukuta maandishi ya vitisho mlangoni kwake leo asubuhi watoto wake walipofungua pazia ya chumba chao wanacholala waliona kitu kikiwa kimefunikwa shuka nyeupe nje ya nyumba yao na ndipo walipomwamsha na alipotoka nje alikuta jeneza hilo ambalo hakujua ni kwa nini liko hapo na nani amelileta.
Alisema aliamua kutoa taarifa kwa majirani na uongozi wa serikali ya kijiji ambapo walipofika walilifunua jeneza hilo la kukuta mifuko ya plastiki inayowekwa nje ya magodoro ya Dodoma yakiwa yamefinywanga pamoja mithili ya kichanga kilichokufa.
Kwa upande wake ofisa mtendaji wa kijiji cha Mkutingome Mussa Bakari  Mbulinda alisema kuwa ni kweli mwalimu huyo amekuwa akitishiwa maisha kila siku kijijini hapo na kwamba tuhuma wanazodai kuwa mwalimu huyo ni mshirikina si za kweli na kwamba wameamua kuitisha mkutano mkuu wa kijiji utakaofanyika siku ya jumatatu April 27 mwaka huu.
Alisema ukweli ni kwamba usalama wa mwalimu huyo uko kwenye mazingira hatarishi na kumuomba mkurugenzi mtendaji wa halmashauri hiyo afanye uhamisho wa mwalimu huyo huku akikiri kuwa hata walimu wengine waliopo kijijini hapo ambao ni wageni waliokuja kuanza kazi kijijini hapo wanaona ni vyema nao wahamishwe wakihofia usalama wa maisha yao na familia zao.
Taarifa za ndani zaidi zinadai kuwa baada ya wanakijiji hao kuona siku walizompa mwalimu huyo aondoke kijijini hapo zimepita waliamua kumletea jeneza ikiwa ni ujumbe kwake kuwa ameshindwa kuondoka kwa ridhaa yake basi ataondoka bila ridhaa yake  akiwa ndani ya jeneza.

MWALIMU Mkuu wa Shule ya Msingi Mkutingome Kata ya Mbekenyera Halmashauri ya Wilaya ya Ruangwa Mkoani Lindi Hemed Ismail Nambea ambaye amekumbwa na kadhia hiyo ya kukuta jeneza nje ya Nyumba yake.
TANGAZO
Facebook Blogger Plugin by WAYEGE CO.LTD
Newer Posts Older Posts
© Copyright Mtazamo Mpya | Designed By FAHARI YA TANZANIA
Back To Top