Loading...
ADVERTISE WITH US ON THIS BLOG.CALL +255 714 789 592/ +255 682 997 767/ +255 752 944 022

Majaliwa Ampa Zawadi Mshindi Wa Insha Afrika Mashariki,Ni Mwanafunzi Kutoka Mbekenyera-Ruangwa

TANGAZO
WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Majaliwa K. Majaliwa.

Na Mwandishi Wetu
WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amesema shule za sekondari za Kata zina fursa ya kufanya vizuri kama zilivyo shule nyingine, licha ya kuwa watu wengi wanazidharau. Alitoa kauli hiyo juzi wakati akikabidhi zawadi ya kompyuta mpakato kwa mwanafunzi aliyeshinda shindano la kuandika insha katika nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).
Kompyuta hiyo ina thamani ya Sh milioni 1.9. Mwanafunzi huyo, Jabir Mandando, amehitimu kidato cha nne katika shule ya sekondari ya Mbekenyera iliyoko wilayani Ruangwa mkoani Lindi. Alipata ufaulu wa daraja la pili na sasa anasubiri matokeo ya kujiunga na kidato cha tano. Mandando aliandika insha hiyo wakati akiwa kidato cha nne mwaka jana.
“Huyu ni mtoto wa kijijini tu. Anatoka kijiji cha Namilema wilaya ya Ruangwa mkoa wa Lindi. Shule ya Mbekenyera aliyosoma ni shule ya Kata. Ameweza kushinda tuzo na kushika nafasi ya tatu katika shindano lililoshirikisha shule nyingi za Jumuiya ya Afrika Mashariki,”alisema.
Alieleza kuwa mwanafunzi huyo licha ya kutoka katika shule ya Kata aliweza kuchomoza kitaifa katika shindano la kimataifa. “Nimeamua kumpa zawadi hii aweze kujisomea zaidi na kupata elimu ya masuala mbalimbali kwa kutumia kompyuta hii. Pia nataka iwe chachu kwa vijana wengine kushiriki mashindano kama haya,” Waziri Mkuu alisema.
Aidha, alimkabidhi Mwalimu Mkuu wa shule hiyo, Shanael Nchimbi fedha taslimu Sh 500,000 zikiwa ni zawadi kwa ajili ya shule hiyo. Mwalimu Nchimbi alimsindikiza mwanafunzi huyo Arusha kupokea zawadi hizo katika mkutano wa Wakuu wa Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), uliomalizika jijini humo wiki iliyopita.
Kwa upande wake, Mandando alimshukuru Waziri Mkuu kwa zawadi na kuahidi kuongeza bidii katika masomo yake ya kidato cha tano na cha sita, ili ndoto yake ya kuwa daktari itimie. Alipoulizwa alipataje taarifa ya uwepo wa shindano hilo, alisema: “Walimu walipata taarifa wakazileta darasani na kutuambia tushiriki kuandika. Walizikusanya na kuchagua tatu bora, ndipo yangu ikashinda.”

TANGAZO
Facebook Blogger Plugin by WAYEGE CO.LTD
Newer Posts Older Posts
© Copyright Mtazamo Mpya | Designed By FAHARI YA TANZANIA
Back To Top