Loading...
ADVERTISE WITH US ON THIS BLOG.CALL +255 714 789 592/ +255 682 997 767/ +255 752 944 022

WAZIRI AAGIZA MILIONI 89 ZIPELEKWE HOSPITALI YA MISHENI YA NDANDA

TANGAZO
Na Clarence Chilumba, Masasi.
Serikali kupitia wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii imemwagiza katibu Tawala mkoa wa Mtwara kwa kushirikiana na mganga mkuu wa mkoa huo kuhakikisha kiasi cha Shilingi  89 milioni zinapelekwa katika hospitali ya rufaa ngazi ya mkoa ya  mtakatifu Benedictine Ndanda .

Akizungumza mwishoni mwa wiki katika ziara yake hospitalini hapo Naibu waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Stephen Kebwe alisema kiasi hicho cha fedha ni kati ya Shilingi milioni 178 zilizotoka hazina na kuelekezwa kwenda katika hospitali hiyo kwa ajili ya mishahara pamoja na mafunzo ya vitendo lakini zilizofika hospitalini hapo ni Shilingi  89 milioni pekee.

Alisema kiasi cha shilingi milioni 89 kati ya hizo ziliishia mkoani Mtwara na kwamba uongozi wa mkoa huo ni lazima wahakikishe kuwa fedha hizo zinapelekwa ili wananchi wanaopata huduma katika hospitali hiyo waweze kuhudumiwa katika mazingira yaliyo bora.

Aidha waziri huyo wa afya na ustawi wa jamii alitumia ziara hiyo kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa maabara ya kisasa unaoendelea hospitalini hapo.

Kebwe alisema pesa yoyote inayotoka hazina kwenda popote nchini ni vyema kabla ya matumizi ziuliziwe ni za kazi gani ili kuepusha kukwama kwa yale mambo yaliyokusudiwa ikiwemo miradi ya maendeleo.

“Namwagiza katibu tawala na mganga mkuu wa mkoa wahakikishe Shilingi 89 milioni zilizokwama mkoani zinakuja Ndanda kama ilivyokusudiwa ili ziweze kutumika mahali ambapo serikali ilipanga fedha hizo zitumike”.alisema Kebwe.

 Alisema Wizara kwa kushirikiana na shirika la afya ulimwenguni (WHO)  liliona kuna umuhimu wa kuboresha huduma za maabara nchini ili ziweze kutoa huduma bora na za uhakika katika kiwango cha kimataifa hivyo ni imani ya serikali kuwa  kukamilika kwa maabara hiyo kutaondoa  utaratibu wa kwenda kupima sampuli za magonjwa kama ebola nje ya nchi.

Awali akisoma risala kwa waziri daktari bingwa wa magonjwa na afya ya watoto, Stanslaus Wambyakale alisema kuwa hospitali hiyo imekuwa ikikabiliwa na uhaba wa fedha za kulipa watumishi, wodi ya watoto wachanga, gari ya kubeba wagonjwa pamoja na watumishi.

Alisema hospitali hiyo ni moja ya hospitali mkoani Mtwara inayohudumia wagonjwa kutoka sehemu mbalimbali za mikoa ya kusini pamoja na nchi jirani ya Msumbiji hivyo wameiomba serikali kuitilia mkazo hospitali hiyo.

Akizungumza mmoja wa wazazi aliyekuwa katika wodi ya watoto hospitalini hapo, Amina Hamis alisema kuwa wamekuwa wakipatiwa huduma kwa wakati pindi wanapofika hospitalini hapo lakini changamoto wanayokumbana nayo ni msongamano wa wagonjwa.

Alisema huduma zitolewazo na hospitali hiyo ni nzuri na kwamba wamekuwa wakilipia michango kidogo tofauti na hospitali zingine kwani wamekuwa wakichangia shilingi 10,000 tu kwa wanaojifungua kwa njia ya kawaida huku wale wanaofanyiwa upasuaji wakichangia shilingi 25,000.

Maabara inayojengwa katika hospitali ya Misheni ya Ndanda mkoani Mtwara ni miongoni mwa maabara saba zilizoteuliwa nchini kwa kufuata vigezo vilivyowekwa na wataalamu wa afya kuingia katika mradi huo.
Mwisho.


TANGAZO
Facebook Blogger Plugin by WAYEGE CO.LTD
Newer Posts Older Posts
© Copyright Mtazamo Mpya | Designed By FAHARI YA TANZANIA
Back To Top