Loading...
ADVERTISE WITH US ON THIS BLOG.CALL +255 714 789 592/ +255 682 997 767/ +255 752 944 022

MAMA KIKWETE ATOA MADAWATI 100 KWENYE SHULE ALIYOWAHI KUFUNDISHA RUANGWA

TANGAZO
Mbunge wa Jimbo la Ruangwa Kassimu Majaliwa.
Na Mwandishi wetu, Ruangwa.
Wazazi na walezi wa watoto wanaosoma kwenye Shule ya Msingi ya Mnacho katika Wilaya ya Ruangwa Mkoani Lindi wametakiwa kuhakikisha kuwa watoto wao wanahudhuria masomo yao na wanapaswa kufuatilia maendeleo yao kitaaluma kwa watoto wao.

Wito huo umetolewa shuleni hapo Jana na Mke wa Rais na Mwenyekiti wa Taasisi ya maendeleo ya wanawake Mama Salma Kikwete kwenye sherehe ya   kukabidhi madawati 100 ambapo amewahimiza wazazi hao kuthamini elimu ya watoto kwani ndio tunu bora kwa maisha ya baadaye ya watoto wao.

Alisema,  akiwa Mwalimu Mwanafunzi alianza kufundisha kwenye shule hiyo na Februari mwaka jana alitembelea shule hiyo na  kukuta upungufu wa madawati mazingira yaliyomfanya  atoe  Milioni 5 na kumkabidhi Mbunge wa Jimbo la Ruangwa,Kasim Majaliwa  ili anunue madawati hayo aliyoyakabidhi.

Akizungumzia juu ya uchaguzi Mkuu ujao Mama Kikwete aliwahamasisha wakazi wa Vijiji vya Tarafa ya Mnacho waliohudhuria sherehe hiyo fupi kuendelea kumpa kura Mbunge Majaliwa kusudi awaletee maendeleo yao katika kipindi cha miaka mitano ijayo.

“Kama Rais amemchagua kuwa Naibu Waziri Tamisemi anayeshughulikia Elimu,ni kitu gani kitawafanya ninyi mshindwe kumchagua Majaliwa kwenye uchaguzi ujao”,aliuliza Mama Kikwete.

Akiyapokea madawati hayo kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Ruangwa,Katibu Tawala,Salvius Kilowoko alimshukuru Mama Kikwete kwa msaada huo ambao utaongeza ari ya wanafunzi kujifunza kutokana na uboreshaji wa miundombinu ya kujifunzia.

Baada ya Kilowoko kuyapokea madawati hayo alimkabidhi Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ruangwa Nikolaus Kombe ambaye alisema “Kwa niaba ya Halmashauri yetu napenda kumshukuru Mke wa Rais kwa kutupatia madawati na nitahakikisha yanatumika kwenye shule hii ya Mnacho na yanatunzwa ipasavyo”

Kwa upande wake Mbunge wa jimbo la Ruangwa Kassimu Majaliwa alimshukuru Mama Kikwete kwa kutimiza ahadi aliyoitoa mwaka jana kwenye shule ambayo yeye alisoma elimu yake ya msingi miaka kadhaa iliyopita, na kumwomba azifikishe kwa Rais Kikwete salamu za matashi mema kutoka kwa Wana-Mnacho.

Kwenye Risala ya Shule hiyo ambayo haikusomwa,Mwalimu Mkuu wa shule hiyo Stephen Ngondo amezitaja changamoto za shule hiyo kama vile,mahitaji ya Madawati 45 na ukosefu wa nyumba za Walimu,kwani kati ya walimu 10 wa Mnacho wenye nyumba ni wawili tu, huku wengine wanane wakiishi nyumba za kupanga.

Changamoto nyingine ni uchakavu wa majengo kwa kuwa yaliyopo yamerithiwa toka kwa Wamisionari wa Kanisa Katoliki waliojenga majengo hayo mwaka 1932 kabla Serikali haijataifisha mwaka 1963.

Kwa upande wa taaluma shule hiyo yenye wanafunzi wapatao 371 wakiwemo wavulana 177 na wasichana 194 ina ukosefu pia wa vitendea kazi kama vile vivunge vya Sayansi, Hisabati pamoja Jiografia unaosababishwa na ruzuku ndogo inayoletwa shuleni hapo.

Sherehe hiyo ilihitimishwa na utoaji wa zawadi ambapo wazazi na walezi ambao watoto wao wanasoma kwenye shule hiyo walimkabidhi Mama Kikwete dume la mbuzi.

Mwisho.


TANGAZO
Facebook Blogger Plugin by WAYEGE CO.LTD
Newer Posts Older Posts
© Copyright 2025 Mtazamo Mpya | Designed By FAHARI YA TANZANIA
Back To Top