Loading...
ADVERTISE WITH US ON THIS BLOG.CALL +255 714 789 592/ +255 682 997 767/ +255 752 944 022

HOSPITALI YA MKOMAINDO YAPEWA MSAADA WA VIFAA KUTOKA KWA MKUU WA MKOA.

TANGAZO
Na Clarence Chilumba,Masasi.
Hospitali ya Mkomaindo iliyopo Halmashauri ya Mji wa Masasi imepewa msaada wa vifaa mbalimbali vitakavyotumika hospitalini hapo kwa wagonjwa kutoka ofisi ya mkuu wa mkoa wa Mtwara.

Vifaa vilivyokabidhiwa kwa mganga mfawidhi wa hospitali hiyo Dkt.Musa Rashidi ni pamoja na mashuka 85,chandarua 55 na ndoo kubwa tano vyote vikiwa na malengo ya kuboresha usafi sambamba na kulinda afya za akinamama na watoto.

Akikabidhi msaada huo jana kwa niaba ya mkuu wa mkoa wa Mtwara,Mganga mkuu wa mkoa wa Mtwara Dkt.Shaibu Maarifa alisema vifaa hivyo ni sehemu ya vifaa vilivyopatikana kutoka kwa wadau mbalimbali wa maendeleo waliochangia wakati wa kilele cha maadhimisho ya siku ya wanawake duniani yaliyofanyika kwenye viwanja vya mashujaa mkoani Mtwara.

Alisema Mkuu wa mkoa wa Mtwara Halima Dendego aliamua kuvigawa vifaa hivyo kwa baadhi ya hospitali zilizopo mkoani humo mkomaindo ikiwemo ili kupunguza za changamoto za upungufu wa vifaa zinazozikabili hospitali hizo mkoani humo.

Kwa mujibu wa mganga mkuu huyo alisema kupatikana kwa vifaa hivyo ni ukombozi kwa hospitali hiyo ambayo kwa kiasi kikubwa ilikuwa na uhaba wa vifaa hivyo hasa mashuka huku akitoa wito kwa wadau wengine mkoani humo kuunga mkono jitihada zinazofanywa na mkuu wa mkoa huo katika kutoa michango mbalimbali kwenye jamii.

Kwa upande wake mganga mfawidhi wa hospitali ya Mkomaindo Dkt.Mussa Rashidi alisema wanaishukuru ofisi ya mkuu wa mkoa wa Mtwara kwa kuwapa msaada huo ambao umefika kwa wakati muafaka kutokana na adha waliyokuwa nayo ya upungufu wa vifaa katika hospitali hiyo.

Alisema licha ya kupokea msaada huo lakini bado wanakabiliwa na changamoto kubwa ya vifaa vikiwemo vitanda kwa ajili ya wagonjwa, uchakavu wa majengo ambayo yamejengwa tangu mwaka 1951 wakati wa ukoloni ambayo kwa sasa hayana hadhi ya kuwa hospitali ya wilaya.

Alisema bado wana upungufu mkubwa wa mashuka licha ya kupewa hayo 85 kwa kuwa mahitaji ni 2050 yaliyopo ni 300 huku upungufu ikiwa ni mashuka 1750 ambapo wamemuomba mkuu wa mkoa kuendelea kuwasaidia katika kuchangia vifaa katika hospitali hiyo pindi vinapopatikana.

Kwa mujibu wa Dkt.Mussa alisema hali si ya kuridhisha katika hospitali hiyo kwani kitaalamu kila kitanda kimoja cha mgonjwa kinahitajika kuwepo na shuka nane na kwamba kwa sasa uwezo wao kila kitanda kina shuka mbili tu mazingira ambayo ni hatari kwa afya za wagonjwa wanaolazwa katika hospitali hiyo.
Mwisho.




TANGAZO
Facebook Blogger Plugin by WAYEGE CO.LTD
Newer Posts Older Posts
© Copyright Mtazamo Mpya | Designed By FAHARI YA TANZANIA
Back To Top