Loading...
ADVERTISE WITH US ON THIS BLOG.CALL +255 714 789 592/ +255 682 997 767/ +255 752 944 022

HOSPITALI YA MKOMAINDO WAIOMBA SERIKALI KUWAJENGEA MAJENGO MAPYA NA YA KISASA

TANGAZO
Mwaka ambao Hospitali Hiyo imejengwa.
Na Clarence Chilumba,Masasi.
Hospitali ya Mkomaindo iliyopo Halmashauri ya MJi wa Masasi mkoani Mtwara imeiomba serikali kuisaidia katika ukarabati pamoja na ujenzi wa baadhi ya miundo mbinu iliyopo hospitalini hapo ili iweze kutoa huduma bora na za kisasa kwa wagonjwa wanaopata huduma katika hospitali hiyo.

Akizungumza na gazeti hili Kaimu mganga mkuu wa Hospitali ya Mkomaindo Dkt.Albano Nditi alisema miundo mbinu mingi ya hospitali hiyo ni chakavu ambayo inahitaji ukarabati kutokana na baadhi ya majengo hayo yaliyojengwa mwaka 1951 kuonekana muda wake umepita  huku baadhi ya majengo yakihitaji kujengwa upya.

Alisema hali ya majengo yaliyopo ya kutolea huduma katika Hospitali hiyo hayaridhishi kwa kuwa mengi ni ya zamani na yamechakaa na kwamba wanaiomba serikali kusaidia katika kufanya ukarabati wa majengo hayo likiwemo jengo la utawala lililojengwa na wakoloni wa kijerumani.

Kwa mujibu wa kaimu mganga mkuu huyo alisema hospitali hiyo pia inakabiliwa na upungufu wa majengo hususani ya kisasa kwa ajili ya kulaza wagonjwa likiwemo jengo la wodi ya kisasa,wodi ya wagonjwa wa dharura,jengo la kulaza wagonjwa wenye milipuko pamoja na jengo la kisasa la kuchomea taka.

Alisema licha ya kupokea msaada wa gari moja la kubebea wagonjwa kutoka kwa mwenyekiti wa taasisi ya maendeleo ya wanawake nchini (WAMA) Mama Salma Kikwete bado  hospitali hiyo inayohudumia wagonjwa wengi wakiwemo wale wa nchi jirani ya Msumbiji ina uhaba mkubwa wa magari kwa ajili ya uendeshaji wa shughuli za huduma za afya katika hospitali hiyo.

Alisema kuwa kwa sasa hospitali hiyo ina magari mawili tu ambayo yote ni ya kubebea wagonjwa  huku magari mengine mawili yakiwa hayafanyi kazi kutokana na ubovu ambao unahitaji matengenezo makubwa ama kubadilishwa kwa magari hayo na kwamba hali ya utendaji kazi hospitalini hapo imekuwa ya kusuasua kutokana na kukosekana kwa usafiri wa uhakika kwa wafanyakazi.

Dkt.Nditi alieleza kuwa kutokana na uhaba wa magari wafanyakazi wa hospitali hiyo wanalazimika kutumia magari ya kubebea wagonjwa kufanya safari mbalimbali za kikazi kitu ambacho amekiri kuwa ni kinyume na maagizo ya wizara ambapo amesisitiza kuwa bado kilio chao wanakilekeza kwa serikali iweze kutatua changamoto hizo.

Alizitaja changamoto nyingine kuwa ni pamoja na kukosekana kwa gari kubwa kwa ajili ya kusafirishia mizigo mbalimbali pamoja na kuhamisha watumishi wa idara hiyo kutokana na gari aina ya Isuzu tani saba lililokuwepo kuchomwa moto wakati wa vurugu zilizotokea januari 2013.

Aidha Changamoto zingine alizozibainisha ni uchache wa fedha kwa ajili ya ununuzi wa dawa kutoka bohari kuu ya madawa (MSD) zinazotolewa na wizara ya afya hivyo kusababisha uhaba wa dawa,ukosefu wa majokofu ya kuhifadhia chanjo kwa ajili ya huduma za afya ya uzazi na mtoto,pamoja na idadi ndogo iliyopo ya watumishi mazingira yanayopelekea huduma kutotolewa kwa wakati.

Akizungumza kuhusu mikakati iliyopo kwa ajili ya kukabiliana na baadhi ya  changamoto hizo kaimu mganga mkuu huyo alisema idara inaendelea kuomba watumishi kutoka wizara ya afya na ustawi wa jamii pamoja na kununua vitanda na shuka kwa awamu pindi fedha itakapopatikana.

Kwa upande wake mwenyekiti wa Halmashauri ya Mji wa Masasi ambaye pia ni diwani wa kata ya Nyasa Andrew Mtumusha alisema Halmashauri itaendelea kufanya ukarabati wa baadhi ya majengo chakavu katika hospitali hiyo pamoja na yale yaliyopo katika vituo vya afya na zahanati kutegemea na upatikanaji wa fedha kutoka kwenye mapato yake ya ndani licha ya kuendelea kuiomba serikali kutoa kipaumbele katika hospitali hiyo kongwe nchini.

Idara ya afya Halmashauri ya mji wa Masasi mkoani Mtwara ina vituo 13 vya kutolea huduma za afya ikwemo hospitali moja ya Mkomaindo,Kituo kimoja cha afya,zahanati 11 huku kwa upande wa watumishi idara hiyo ina madaktari watano tu huku mahitaji yakiwa ni madaktari 25 ambapo pungufu ni madaktari 20.

Mwisho.
TANGAZO
Facebook Blogger Plugin by WAYEGE CO.LTD
Newer Posts Older Posts
© Copyright 2025 Mtazamo Mpya | Designed By FAHARI YA TANZANIA