Loading...
ADVERTISE WITH US ON THIS BLOG.CALL +255 714 789 592/ +255 682 997 767/ +255 752 944 022

TANGAZO
DC AAPA KULA SAHANI MOJA NA WAZAZI PAMOJA NA VIONGOZI WAZEMBE

Mkuu wa wilaya ya masasi mkoani Mtwara  Farida Mgomi ametoa onyo kali kwa  wazazi wa watoto waliochaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza kwa mwaka wa masomo wa 2014/2015 kuwa hatosita kuwachukulia hatua kali za kisheria ikiwa ni pamoja na kuwafikisha mahakamani wazazi hao watakaothubutu kuacha kuwapeleka watoto wao shuleni.
Pia ametoa agizo kwa   watendaji wa kata na vijiji wilayani humo kufuatilia chanzo cha wanafunzi wengi kutoripoti shuleni bila sababu za msingi huku akiwapa rai  kuwa endapo baadhi yao watabainika kuwa ni  sababu ya  utoro huo kwenye maeneo yao basi wajiandae kutafuta kazi zingine zitakazowafaa kabla hajawachukulia hatua kali.  
Aidha alisema inashangaza na inatia aibu kwa wilaya ya Masasi ambayo imetoa viongozi wengi wa kitaifa huku ikiwa haina tatizo la vyumba vya madarasa kuona kuwa idadi kubwa ya wananfunzi wanaochaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza kila mwaka huwa hawaripoti shuleni kutokana na uzembe wa baadhi ya wazazi.
Aliyasema hayo jana wakati wa mahojiano maalumu na gazeti hili lililotaka kufahamu wilaya ya Masasi imejipangaje katika kukabiliana na idadi kubwa ya wanafunzi ambao kila mwaka huchaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza lakini cha kushangaza wengi wao hawaripoti kwa kisingizio kutoka kwa wazazi wao cha hali ngumu ya maisha.
Alisema wazazi waache kutoa visingizio visivyo na mantiki yoyote vya kukosa uwezo wa kuwapelekea watoto wao shuleni huku wakitumia pesa nyingi wakati watoto hao wanapomaliza shule ya msingi kwa kuandaa chakula, mavazi ya gharama pamoja na pombe wakifurahia watoto wao kumaliza elimu ya msingi.
“Ni jambo la kushangaza na linalosikitisha kwa baadhi ya wazazi wilayani Masasi ambao wamekuwa na tabia ya kutumia fedha nyingi wakati ule watoto wao wanapomaliza elimu ya msingi…lakini kipindi cha watoto hao kuwapeleka sekondari wazazi hao hushindwa kumudu gharama hizo kwa kisingizio cha hali ngumu ya maisha na kwamba kwa hili halipaswi kuvumiliwa ni lazima mwaka huu tulikomeshe”.Alisema.
Mgomi alisisitiza kuwa wilaya ya Masasi haina tatizo la vyumba vya madarasa na kwamba wanafunzi wote wapatao 3897 waliochaguliwa kujiunga na kidato kwa kwanza mwaka huu   wote watapata nafasi ya kusoma.
Alisema hatomuonea haya mzazi yeyote ama kiongozi yeyote yule ambaye kwa namna moja ama nyingine atachangia kuzorotesha jitihada za wilaya ya Masasi za kuhakikisha kuwa watoto wote wanaripoti shuleni ifikapo januari 31, 2015 na kwamba ameapa kula nao sahani moja ili iwe fundisho kwa wengine.
 Wakizungumza kwa nyakati tofauti wenyeviti wa Halmashauri zinazounda wilaya ya Masasi Andrew Mtumusha ambaye ni mwenyekiti wa Halmashauri ya mji wa Masasi pamoja na Juma Satma wa Halmashauri ya wilaya ya Masasi walikiri kuwa tatizo hilo Masasi ni kubwa na kwamba hawaelewi ni kwa nini wazazi wengi wilayani humo hawatambui umuhimu wa elimu wakati wamekuwa wakitumia fedha nyingi kwenye sherehe kama vile jando na unyago pamoja na harusi.
Walisema bado msimamo wao ni kuwataka wazazi ambao watoto wao wamechaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza mwaka huu wawapeleke shuleni na kwamba mzazi ambaye atakiuka amri hiyo ambayo ni ya kisheria basi hatua kali zitachukuliwa dhidi yake.
Walisisitiza kuwa  wakati umefika  kwa madiwani wa halmashauri hizo mbili  kutambua kuwa hilo ni jukumu lao na kwamba wanapaswa kutoa msukumo mkubwa  ikibidi kutumia nguvu kwenye maeneo yao katika kupambana na baadhi ya  wazazi ambao wamekuwa ni kikwazo  ili kukinusuru kizazi hiki kinachoelekea kupotea kwa kukosa elimu.
“Sisi Kama wenyeviti wa Halmashauri hizo tayari tumejiwekea mikakati madhubuti ikiwa ni pamoja na kuunda kikosi kazi kitakachofanya operesheni maalumu ya nyumba kwa nyumba ili kuwasaka wale wote watakaosababisha wanafunzi hao kutoripoti shuleni kwa wakati”.Walisema.
Wakitoa maoni yao baadhi ya wananchi waliozungumza na gazeti hili  wilayani Masasi  kuhusu sababu ambazo husababisha wanafunzi wengi kutoripoti shuleni wengi wao waliinyooshea kidole idara ya mahakama kwa kile walichodai kuwa  imekuwa ikidhoofisha jitihada zinazofanywa na watendaji wa serikali za vijiji na kata  kwa kutowachukulia hatua kali za kisheria  wazazi ama walezi wanaosababisha watoto wao kutoripoti shuleni.
Waliendelea kusema idara ya mahakama imekuwa ikifanya kazi zake kwa dharau kubwa kwa watendaji hao wa ngazi ya vijiji na kata kwa kuwaachia huru watuhumiwa ambao wamethibitika kusababisha wanafunzi kutoripoti shuleni bila maelezo na kwamba wakati mwingine hutoa majibu yanayokatisha tamaa kuwa hakuna kifungu chochote cha sheria kilichoainisha kwamba anayesababisha mwanafunzi asiende shuleni apewe adhabu.
Walisema mbaya zaidi hata wale wanaowapa ujauzito watoto hao wamekuwa wakiachwa huru licha ya watendaji hao kuwafikisha watuhumiwa kwenye vyombo vya maamuzi mazingira huku baadhi ya wazazi nao wakiingia lawamani kwa kuchukua fedha kidogo kutoka kwa watuhumiwa.
Takwimu zinaonesha kuwa kila mwaka wilaya ya Masasi mkoani Mtwara yenye jumla ya shule 35 za sekondari imekuwa ikifaulisha kwa kiwango cha juu huku wanafunzi wengi wakichaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza lakini changamoto kubwa inayopaswa kutafutiwa ufumbuzi ni ya wanafunzi hao kutoripoti shuleni huku kundi kubwa la watoto hao hasa wa kike likielekea Dar es salaam kwa ajili ya kufanya kazi za ndani.

Mwisho.
TANGAZO
Facebook Blogger Plugin by WAYEGE CO.LTD
Newer Posts Older Posts
© Copyright Mtazamo Mpya | Designed By FAHARI YA TANZANIA
Back To Top