Loading...
ADVERTISE WITH US ON THIS BLOG.CALL +255 714 789 592/ +255 682 997 767/ +255 752 944 022

TANGAZO

AUAWA KWA KUPIGWA MAWE NA HATIMAYE KUCHOMWA MOTO
Na Clarence Chilumba, Ruangwa
Mkazi wa kitongoji cha Mnele kijiji cha Chinongwe B katika kata ya Chinongwe wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi Longino John (35) ameuawa na wananchi wenye hasira kali kwa kupigwa mawe na hatimaye kuchomwa moto kwa madai ya kumpiga na kumjeruhi Mendrati Chinguile (63) ambaye ni mlemavu wa macho.
Tukio hilo la kusikitisha limetokea jana majira ya saa 7:00 mchana huko kwenye kitongoji cha Mnele kilichoko katikati ya kijiji cha Chinongwe na Luchelegwa wilayani Ruangwa ambapo kundi kubwa la watu wenye hasira walimpiga mawe kijana huyo na hatimaye kumchoma moto kwa kutumia mafuta ya petroli.
Akithibitisha kutokea kwa tukio hilo kamanda wa polisi mkoa wa Lindi Renatha Mzinga alisema jana majira ya saa 7:00 mchana kijana huyo aliuawa na wananchi hao wa kitongoji cha Mnele kwa madai ya kuchoshwa na tabia yake ya ubabe aliyokuwa nayo marehemu hasa pale alipokuwa amelewa.
Alisema kabla ya kifo chake marehemu alikuwa ni mtu wa matukio ya ajabu kijijini hapo ikiwemo ulevi wa kupindukia, wizi pamoja na matukio yake ya kupiga watu bila sababu za msingi na kwamba juzi (Alhamisi) alimpiga kwa mapanga na kumjeruhi kichwani mtoto wa mzee Mendrati Chinguile aitwaye Amosi Cleophas (25) na kukimbizwa katika hospitali ya misheni ya Ndanda na hatimaye aliruhusiwa na hali yake inaendelea vizuri.
Mzinga alisema jana asubuhi majira ya saa 2:00 akiwa amelewa marehemu alienda nyumbani kwa mzee Mendrati Chinguile ambaye ni mlemavu wa macho tangu miaka ya 1990 na kwamba alipofika alianza kudai kuwa amekuja kufuata vyombo vyake vya ndani ambavyo kwa mujibu wa mashuhuda walidai kuwa ni taarifa za uzushi na kwamba hakuwa anamdai chochote mzee huyo bali ni hasira ambazo alikuwa nazo dhidi ya mtoto wa mzee huyo.
Alisema malumbano hayo baina yake na mzee huyo yaliendelea bila mafanikio yoyote na hatimaye aliamua kuingia ndani na kumtoa nje ya nyumba yake mzee Mendrati na kuanza kumpiga kichwani kwa kutumia kipande kikubwa cha mti alichokuja nacho mazingira yaliyomsababishia mzee huyo majeraha makubwa kichwani na alikimbizwa na wasamaria wema katika hospitali ya Ndanda na kupata matibabu huku hali yake ikiwa bado inaendelea kuimarika.
Kwa mujibu  wa kamanda mzinga alisema wasamaria wema ndio waliomuokoa mzee huyo asiuawe na kijana huyo kwa kuwa nyumba yake iko nje kidogo na kijiji na kwamba mara baada ya kumkamata walianza kumpiga kwa mawe na hatimaye walifanikiwa kumuua na ndipo waliamua kuchukua mafuta ya petrol kutoka kwa waendesha bodaboda na hatimaye walifanikiwa kumchoma kwa moto.
Alisema polisi walifika eneo la tukio majira ya saa 11:jioni na baada ya kufanya mahojiano na baadhi ya  watu kijijini hapo waliamuru mwili wa marehemu Longino John uzikwe na majira ya saa 12:30 jioni marehemu alizikwa na watu wachache waliofika kwenye eneo hilo na kwamba hadi sasa hakuna mtu yeyote anayeshikiliwa na jeshi la polisi huku upelelezi ukiendelea wa kuwabaini waliofanya tukio hilo la kinyama.

Mwisho.
TANGAZO
Facebook Blogger Plugin by WAYEGE CO.LTD
Newer Posts Older Posts
© Copyright Mtazamo Mpya | Designed By FAHARI YA TANZANIA
Back To Top