Loading...
ADVERTISE WITH US ON THIS BLOG.CALL +255 714 789 592/ +255 682 997 767/ +255 752 944 022

WATU 82,795 WAANDIKISHWA KWENYE DAFTARI LA KUDUMU LA WAPIGA KURA WILAYANI RUANGWA

TANGAZO
Na Clarence Chilumba,Ruangwa.
JUMLA ya wananchi 82,795 ambao ni sawa na asilimia 99 katika wilaya ya Ruangwa mkoani Lindi wamejiandikisha kwenye daftari la kudumu la wapiga kura kwa kutumia mfumo wa kielektroniki wa BVR kwa ajili ya kushiriki kwenye uchaguzi mkuu pamoja na kuipigia kura ya ndio au hapana katiba inayopendekezwa.
Akitoa taarifa jana ya zoezi la uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura kwa baraza la madiwani la Halmashauri ya wilaya ya Ruangwa mkurugenzi wa Halmashauri hiyo Nicholaus Kombe alisema Halmashauri ya wilaya ya Ruangwa yenye jimbo moja la uchaguzi la Ruangwa lilianza zoezi la uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura April 24 mwaka huu na kumalizika Mei 25.
 Alisema zoezi hilo wilayani humo lilidumu kwa muda wa siku 28 za kazi ukiondoa siku za kuhamisha maofisa waandikishaji na wataalamu wa BVR pamoja na vifaa toka kanda moja kwenda kanda zingine zilizotengwa ndani ya jimbo hilo la uchaguzi.
Alisema uandikishaji ulifanyika ndani ya siku saba katika kila kanda kama ilivyoelekezwa na tume ya Taifa ya uchaguzi ambapo wilaya hiyo ilikuwa na kanda nne za uandikishaji zilizokuwa na jumla ya vituo 182 vya uandikishaji.
Kwa mujibu wa Kombe alisema lengo la uandikishaji katika Halmashauri ya wilaya ya Ruangwa lilikuwa ni kuandikisha watu 83,672 kwa mujibu wa sensa ya ofisi ya takwimu ya Taifa (National Bureau of Statistics-NBS 2015) ambapo watu walioandikishwa ni ni 82,795 sawa na asilimia 99.
Alisema kutokana na takwimu hizo ni dhahiri kuwa zoezi hilo la uandikishaji wilayani humo limevuka lengo ambapo hakusita kuwapongeza madiwani pamoja na viongozi wote wa serikali na vyama vya siasa ambao katika kipindi chote walitoa ushirikiano sambamba na kutoa elimu kwa wananchi umuhimu wa kujiandikisha kwenye daftari la kudumu la wapiga kura.
Akizungumzia kuhusu ushiriki wa vyama vya siasa katika zoezi hilo mkurugenzi huyo alisema kila chama cha siasa chenye usajili wa kudumu kiliruhusiwa kuweka wakala mmoja kwa kila kituo kwa mujibu wa sheria za uchaguzi ambao kwa kushirikiana na waandishi wasaidizi wa vituo walifanya kazi ya kutambua wakazi na kutoa taarifa juu ya watu wasio na sifa ya kuandikishwa.
Alisema kwa ujumla zoezi hilo lilienda vizuri licha ya kuwepo kwa changamoto mbalimbali ambazo kwa kushirikiana na wataalamu kutoka tume ya Taifa ya uchaguzi walifanikiwa kufanikisha mchakato huo muhimu kwa watanzania hasa katika kipindi hiki kuelekea kwenye uchaguzi mkuu wa Rais,wabunge na madiwani.

Mwisho.
TANGAZO
Facebook Blogger Plugin by WAYEGE CO.LTD
Newer Posts Older Posts
© Copyright Mtazamo Mpya | Designed By FAHARI YA TANZANIA
Back To Top